Mchezaji wa timu ya taifa ya Nigeria, Asisat Oshoala alishinda taji la tatu kuwa mchezaji bora Afrika kwa kina dada, usiku wa Alhamisi.
Oshoala alitwaa tuzo hilo mwaka wa 2014 na 2016, na hapo jana aliwapiku Gabrielle Aboudi Onguene wa Cameroon na Chrestina Kgatlana wa Afrika Kusini, katika hafla iliyoandaliwa kule Accra, Ghana.
Oshola ambaye alitwaa taji la BBC mwaka wa 2015, kama mchezaji bora Afrika kwa wanawake, anachezea klabu ya Dalian Quanjian ya China.
Oshoala alihamia klabu hiyo inayoshiriki ligi kuu ya China, mwanzoni mwa msimu uliopita baada ya kupata wakati mgumu katika timu za Liverpool na Arsenal Ladies.
Katika msimu wake wa kwanza kwenye Super League huko Uchina, Oshoala alicheka na wavu mara kumi na mbili ikiwemo mabao mawili katika mechi ya mwisho ya msimu.
Ushindi huo uliisaidia Quanjian kutwaa ligi hiyo pamoja na vikombe vingine viwili. Oshoala alituzwa taji mshambulizi bora wa ligi hiyo.